Friday, April 25, 2014

'Tekelezeni Majukumu kwa Wakati' - Dk Shein

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
    Zanzibar                                                                                                            25 Aprili , 2014
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amezikumbusha Wizara na Idara za Serikali kutekeleza majukumu yake kwa wakati na kuripoti kwa mamlaka husika ili matokeo yaweze kutolewa kwa wananchi.
“Hatujifanyii sisi bali wananchi tunaowahudumia hivyo hatuna budi tufanye kazi kwa wakati na kutoa taarifa za utekelezaji huo kwa mamlaka husika ili wananchi waweze kuelezwa matokeo ya utekelezaji huo” Dk Shein alisisitiza.
Akihitimisha kikao cha kujadili utekelezaji wa Mpangokazi wa Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano kwa kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014 Ikulu jana Dk. Shein alisisitiza umuhimu kwa Wizara na Idara za Serikali kutumia mamlaka zinazoongoza Wizara na Idara za Serikali kujadili masuala yao na kuyachukulia hatua.
“Kukutana na kushauriana ndio njia pekee ya kufanyakazi kwa ufanisi na kutoa matokeo mazuri” Dk. Shein alieleza na kusisitiza mashauriano kati ya wizara na Bodi zinazosimamia taasisi za Serikali kuwa ni lazima yafanyike mara kwa mara na kutoa taarifa katika mamlaka zilizo juu yake.
Dk. Shein alibainisha kuwa wajibu wa bodi hizo ni kuzisaidia wizara kusimamia taasisi zilizo chini yake kwa mujibu wa Sheria na taratibu zilizowekwa hivyo mawasiliano ya mara kwa mara na wizara ni kitu cha lazima.
“Idara zinaripoti kwa Wizara na Wizara zinaripoti Baraza la Mapinduzi”alisema na kusisitiza kuwa huo ndio utaratibu unaopaswa kufuatwa ili shughuli za Serikali ziweze kufanyika kwa wakati na kwa ufanisi.

Katika kikao hicho Mhe Rais aliziagiza Wizara za Serikali kuvipatia nyenzo vitengo vya Ukaguzi wa Ndani kwa mujibu wa mahitaji na uwezo wa fedha uliopo ili vitengo hivyo viweze kutekeleza majukumu yake kikamilifu na kwa uhuru.  
Awali akiwasilisha Taarifa ya Utekelezaji Mpangokazi wa Wizara hiyo Katibu Mkuu Dk.  Juma Malik Akil alieleza kuwa katika kipindi husika Wizara yake ilipanga kutekeleza miradi ya maendeleo 14 inayojumuisha ujenzi wa barabara, miundombinu ya viwanja vya ndege na bandari pamoja na mradi wa mageuzi ya mfumo wa taasisi.
Alifafanua kuwa miradi hiyo imezingatia utekelezaji wa mipango mikuu ya maendeleo ya nchi ikiwemo Dira ya Taifa ya Maendeleo 2020, Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini-MKUZA II, Sera ya Usafiri Zanzibar, Sera ya TEHAMA na Mpango Mkuu wa Usafiri Zanzibar (Zanzibar Transport Masterplan 2009).
Kwa upande wa ukusanyaji mapato, Dk Akil alieleza kuwa hadi mwezi Machi 2014 Wizara yake imeweza kukusanya jumla ya shilingi milioni 306 ikiwa ni asilimia 75 ya lengo la Wizara hiyo la kukusanya shilingi milioni 406 kwa mwaka wa fedha wa 2013/2014.

Postal Address: 2422 Tel.+255 776 613 015, Fax: 024 2231822 

0 comments:

Post a Comment