Wednesday, December 18, 2013

Mbunge Chadema ambana Naibu Waziri, ni kuhusu kauli yake ya wananchi kutumia vibatari

MBUNGE wa Iringa Mjini Mchungaji Peter Msigwa (Chadema), ameitaka Serikali itolee tamko juu ya kauli ya Naibu Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene ya kuwataka Watanzania wasioweza kumudu bei mpya ya umeme watumie vibatari.

Katika swali lake la nyongeza alilouliza kwa niaba ya Mbunge wa Maswa Mashariki Sylvester Kasulumbayi (Chadema), Msigwa alitaka kujua Serikali inaichukuliaje kauli hiyo ya kuwataka wananchi kutumia vibatari iwapo watashindwa kulipia bei mpya ya umeme.

Akijibu swali hilo, Simbachawene alikanusha kutoa matamshi hayo ya kuwataka wananchi kutumia vibatari na kufafanua kuwa kamwe hawezi kudharau matumizi ya taa hiyo ya asili, kwa kuwa ndio iliyomkuza.

Alikiri kuhojiwa na Redio One Novemba 25, mwaka huu, kuhusu suala la kupanda kwa bei ya umeme, ambapo akiwa kama mmoja wa watoa maamuzi, hakutaka kuzungumzia ukweli kuwa bei hiyo inapanda au la.

“Nasikitika nilinukuliwa vibaya na baadhi ya vyombo vya habari, niliposikia taarifa hii niliomba mkanda wa mahojiano yangu kwa uongozi wa Redio One na kuyasikiliza ukweli ni kwamba maneno haya hayamo, naomba Watanzania watambue kuwa walipotoshwa,” alisisitiza Simbachawene.

Alisema alichoulizwa katika mahojiano hayo, ni kama mwananchi wa kawaida ataweza kulipia gharama za umeme za bei hiyo mpya kutokana na maisha magumu yaliyopo sasa.

Alisema katika majibu yake, alikwepa kukiri kuwa bei ya umeme inapanda au la, ila alitumia neno kibatari wakati akilinganisha gharama halisi za matumizi ya umeme wa kawaida na gharama za anayetumia nishati ya kibatari.

“Nilifafanua kuwa mtumiaji wa kibatari ndiye mwenye gharama kubwa kutokana na mafuta ya taa anayonunua kila siku, wakati yule wa umeme hutumia gharama nafuu kwa kulipia mara moja kwa mwezi gharama ya Sh 1,500 kwa uniti, hii ndio dhana yangu ya kutumia neno kibatari, siwezi kukashifu matumizi yake hata kidogo,” alisema.

Katika swali la msingi la Kasulumbayi, alitaka kujua asilimia 35 ya pato la Watanzania wa kipato cha chini inayotumika kwenye nishati imepanda au kushuka na iwapo uvumbuzi wa visima vipya vya gesi asilia vimesaidia matumizi ya nishati kwa Watanzania wenye kipato kidogo.

Akijibu swali hilo, tangu kutolewa kwa takwimu hiyo mpya ya pato la mwananchi mwenye kipato cha chini ni muda mrefu na sasa inahitajika takwimu mpya ambapo wizara hiyo kwa kushirikiana na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Ofisi ya Taifa ya Takwimu itafanya utafiti kwa nchi nzima ili kupata kiwango kipya cha takwimu hizo.

Kuhusu uvumbuzi wa gesi asilia, Simbachawene, alisema kutokana na taarifa ya upembuzi yakinifu, mradi wa kusambaza gesi asilia jijini Dar es Salaam utahusisha kaya 30,000, magari 8,000 ambayo yatajaza gesi kupitia vituo 15 vya gesi pamoja na hoteli 10.

Alisema gharama za mradi kwa sasa ni dola za Marekani milioni 65.1 na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limemwajiri mwekezaji wa kudurusu upembuzi uliofanyika awali ili kupata gharama halisi pamoja na kusanifu michoro ili mradi ujengwe.

0 comments:

Post a Comment