WATU watatu wamewasilisha ombi kutaka
Mahakama ya Afrika Mashariki isitishe uamuzi
uliopitishwa katika vikao vitatu vilivyofanyika Uganda, Rwanda na Kenya wakidai
vimekiuka mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
Vikao hivyo viliofanyika Entebe, Uganda, Kigali , Rwanda na Mombasa , Kenya .
Walalamikaji wameomba mahakama ionye nchi husika ambazo ni Rwanda, Uganda na Kenya
zisirudie kosa.
Waliofungua kesi ni Ally Msangi,
David Mataka na John Bwenda, ambao wamewasilisha maombi hayo kupitia Wakili
Mwandamizi, Jimmy Obed wa Kampuni ya Uwakili ya Jimmy Obed ya Jijini Dar es
Salaam.
Akizungumza mara baada ya
kuwasilisha maombi hayo kwenye ofisi ya Masijala ya
Mahakama ya Afrika Mashariki Jijini
Arusha na kupokewa na Ofisa Masijala, Boniface Ogotu, Jimmy alidai wanataka mahakama
itamke kuhusu kuheshimu mkataba uliopo .
Alidai Rwanda, Uganda na Kenya
wamekiuka mkataba wa Jumuiya hiyo kupitia vikao walivyofanya Juni 24 na 25
mwaka huu Entebe, Uganda.
Wanadai vikao vingine vilivyofanyika
kinyume na mkataba ni vya Agosti 28 mwaka huu Mombasa, Kenya na Oktoba 28 mwaka huu Kigali, Rwanda.
Alidai katika vikao hivyo walitoa uamuzi
ambao unatakiwa kutekelezwa, na kwamba wamevunja Ibara ya 71(F), 71(D) na Ibara
ya 12 kifungu cha 3 (3)c, Ibara ya 6 (a), (b), (d) na (f) na ibara ya 8 (1) c
na 8 (3)c.
"Wadai wanataka Mahakama hii
ifanyie kazi vizuri maombi haya na kutoa amri ya kuzuia kufanyika kwa
utekelezaji wa uamuzi uliopitishwa kwenye vikao hivyo na kuwaamuru wasirudie kukiuka
mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki''.
Alidai wajibu maombi katika kesi
hiyo ni Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mwanasheria Mkuu wa Kenya,
Uganda na Rwanda.
SOMA: HABARILEO ONLINE








0 comments:
Post a Comment