Wednesday, November 20, 2013

REA Kusambaza Umeme katika Wilaya Sita Morogoro




WAKALA wa Umeme Vijijini ( REA) unatarajia kutekeleza awamu ya pili ya kusambaza nishati hiyo kwenye  wilaya sita za mkoa wa Morogoro kwa gharama ya Sh bilioni 21.5  katika mwaka wa fedha 2013/2014.
Miradi hiyo iliyo kwenye mchakato wa kupata wakandarasi imepangwa kuanza kukelezwa mwezi ujao. Vijiji zaidi ya 30 vilivyo katika  Wilaya
za Gairo, Kilombero, Ulanga, Mvomero, Kilosa na Halmashauri ya wilaya ya Morogoro vitanufaika.

Meneja wa Shirika la Umeme (Tanesco) Mkoa wa Morogoro, Deogratias Ndamugoba, alisema hayo  juzi kwenye taarifa yake kwa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo.
Waziri Muhongo alikwenda kuzindua mradi wa Rea katika Kijiji cha Berega kilichopo wilayani Kilosa.
Alisema miradi ya umeme ya Rea awamu ya kwanza, katika mkoa wa Morogoro inatekelezwa wilaya ya Kilosa, Ulanga na Kilombero.
Vijiji vya wilaya ya Kilosa vilivyonufaika katika awamu ya kwanza na wilaya kwenye mabano ni Kwambe, Maguha, Magumbike, Kiyengea, Gongoni, Mgugu, Berega, Mbegesela, Kisanga, Tazama, Kisanga, Kidodoo, Msolwa Sekondari na Msolwa.
Wilayani Ulanga vijiji vinavyonufaika ni pamoja na Mzelezi, Chilombola, Mwaya, Ruaha, Ngoheranga, Kiswago, Tanga, Mwembeni, Malinyi, Sofi, Manda Juu, Mtimbira, Kipenyo na Itete.
Kwa upande wa wilaya ya Kilombero, vijiji vilivyonufaika ni Mpanga Misheni,  Utengule, Ngalimila na Kisawasawa. Miradi yote imegharimu Sh bilioni 14.8.
Wakati huo huo, wananchi wa vijiji vilivyopitiwa na miradi hiyo ya  Rea  wameipongeza serikali ya awamu ya nne kuwapunguzia gharama ya kuunganisha umeme  katika makazi yao.
Wananchi hao walitoa pongezi hizo kwa nyakati tofauti mbele ya Waziri Muhongo, ambaye alifanya ziara kwenye vijiji vilivyo kwenye mpango wa awamu ya kwanza ya kupatiwa umeme wa  Rea.
Wakazi wa Kijiji cha Mtombozi waliozungumza na mwandishi wa habari hizi,  walisema serikali imewapa faraja kutokana na kuwaunganishia umeme.
Serikali imetupa faraja sisi wananchi wa vijijini, kwani tunatambua umuhimu wa umeme katika kutuletea maendeleo yetu ya kiuchumi na kuboresha huduma za kijamii kama afya na elimu, alisema Zainabu Salum.
Kwa upande wake,  Paroko wa Parokia ya Bunduki, Padri Godfrey Lembele akizungumza mbele ya Waziri Muhongo, alisema kufikishwa umeme katika kijiji cha Bunduki, tarafa ya Mgeta kutawezesha  wananchi kukuza kipato.
Alisema hayo ni mapinduzi makubwa ya kuondokana na umaskini kupitia  nyanja mbalimbali za kimaendeleo.
Mkurugenzi wa Hospitali ya Beraga inayomilikiwa na Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Morogoro, Mchungaji  Isaac Mgego, alisema wamepunguziwa  gharama ya matumizi ya mafuta
ya kuendeshea jenereta  ambapo kwa mwezi walikuwa wakitumia Sh milioni
moja.
Tunaishukuru Serikali, imetimiza ahadi yake iliyotolewa na Rais Mstaafu Benjamini Mkapa, alisema Mchungaji Mgego.
 Hospitali ya Berega ilianzishwa na wamisionari wa kanisa hilo mwaka 1879 ambapo umeme umeingizwa miezi mitatu iliyopita.

Katika mikutano yake ya hadhara kwenye vijiji alivyotembelea, Waziri aliwaambia wananchi serikali  imepunguza gharama za kuingiza umeme vijijini na kuwa Sh 177,000.

Alishauri wananchi kutumia fursa hiyo kwa kulipa kwa awamu wanufaike na umeme utakaokuza  uchumi wao  kupia ya kilimo, biashara na uanzishwaji wa viwanda vidogo vidogo vijijini.

0 comments:

Post a Comment