TAARIFA KWA VYOMBO VYA
HABARI
KAULI YA WAZIRI KIVULI
WA VIWANDA NA BIASHARA KUHUSU EFD
Tangu
mwishoni mwa mwaka jana, mwezi Novemba na mapema mwanzoni mwa mwaka huu,
Serikali hususan kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), imekuwa kwenye
mgogoro mkubwa na wafanyabiashara kuhusu matumizi ya vifaa vya kielektroniki
kwa ajili ya kutoza na kukusanyia kodi (EFD).
Mgogoro huo
umekuwa mkubwa kiasi kwamba wafanyabiashara katika maeneo mbalimbali ya nchi,
kupitia katika jumuiya zao, waliamua kufanya maandamano na kufunga maduka yao
kama moja ya njia za kuwasilisha madai yao serikalini ili yaweze kufanyiwa
kazi.
Miongoni mwa
madai ya wafanyabiashara hao dhidi ya serikali ni pamoja na;
·
Elimu
juu ya matumizi ya EFD, hali ambayo inaonesha hakukuwa na maandalizi wala ushirikishwaji
wa wadau wote katika suala hilo muhimu.
·
Kuwepo
kwa hali ya kulazimishwa kwa watu wasiohusika kwa maana ya wafanyabiashara
wenye mitaji midogo ukilinganisha na gharama za kununua na kuendesha mashine
hizo.
·
Bei
kubwa ya kununulia na kuendesha mashine hizo, ambayo inasababishwa na
upatikanaji wake ikidaiwa kuwa kuna msambazaji mmoja tu.
Ndugu
wanahabari
Kama
mnavyojua, suala hili ni mtambuka. Linahusisha sekta nyingi na zaidi ya wizara
moja. Wizara mama ya wafanyabiashara nchini ni Wizara ya Viwanda na Biashara
huku suala la matumizi ya EFD likiwa chini ya Mamlaka ya Mapato (TRA) iliyoko
chini ya Wizara ya Fedha na Uchumi.
Wizara zote
hizo mbili hadi sasa zimeshindwa kutoa suluhisho katika mgogoro huu ambao sasa
unaanza kutishia mzunguko wa uchumi na bila shaka kama utaendele namna hii
unaweza kusababisha mfumuko wa bei ambapo hatimaye mwathirika atakuwa ni
mwananchi wa kawaida au mtumiaji wa mwisho wa bidhaa na huduma za wahusika wote
katika sakata hili.
Kutokana na
ukweli kwamba wizara zote hizo mbili zimeshindwa kutoa majawabu ya kumaliza
kabisa kadhia hiyo inayoendelea kati ya wafanyabiashara na TRA, tunataka mambo
kadhaa yafanyike.
·
Kwa
hatua ambayo mgogoro huu umefikia na namna unavyochukua sura mpya kila siku,
sasa serikali itambue kwamba hili tayari ni tatizo ambalo linahitaji suluhisho
na majawabu sahihi.
·
Serikali
iache kutumia mabavu, vitisho vya kutumia polisi na kauli za kejeli katika
kushughulikia tatizo hilo, hasa kupitia kwa wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya.
·
Serikali
iweke wazi mchakato uliotumika kumpata muuzaji na msambazaji wa hizo mashine za
EFD.
·
Serikali
iweke wazi mkataba uliopo kati yake na muuzaji/ msambazaji wa mashine za EFD.
·
Serikali,
kupitia Ofisi ya Rais (Ikulu), itoe ufafanuzi wa namna ambavyo madai hayo ya
wafanyabiashara yatafanyiwa kazi ili shughuli za uuzaji, uzalishaji na utoaji
huduma ambayo ni sehemu ya mzunguko wa uchumi, ziendelee huku kila mtu
akitimiza wajibu wake, kwa maana ya mtoa kodi, mkusanya kodi na mtoza kodi kwa
ajili ya maendeleo ya taifa letu.
Tunaitaka
ikulu ijitokeze kumaliza mgogoro huu kwa sababu tayari suala hilo limefika huko
baada ya wafanyabiashara wenyewe kumwandikia barua Rais Jakaya Kikwete aingilie
kati kusaidia kuondoa utata.
Kuna umuhimu
wa Rais Kikwete kuwaambia Watanzania hatima ya tatizo hilo kwa sababu
kimantiki, wafanyabiashara wameamua kuchukua hatua hiyo baada ya wizara zote
mbili kuishia kutoa ahadi na matumaini hewa ya kushughulikia lakini hakuna kitu
chochote kinachoendelea.
Tunatambua
umuhimu wa kuwepo na mfumo mzuri utakaohakikisha kuwa kila mtu anayestahili
kulipa kodi anafanya hivyo kadri ya kanuni za ulipaji kodi zilivyo, hivyo
hatuwezi kukubali kuwepo mianya yoyote yoyote ile ya watu kukwepa kodi.
Tumelisema hili mara kadhaa na tutaendelea kusisitiza.
Pamoja na
kusisitiza umuhimu wa ulipaji kodi, tutaendelea pia kuhoji busara inayotumika
kuweka ‘vihunzi’ vingi sana kwa makundi fulani ya walipa kodi, huku serikali
hiyo hiyo ikiendelea kutoa mianya ya kukwepa kodi au kutoa misamaha mikubwa ya
kodi kwa wafanyabiashara au wawekezaji wakubwa kiasi hata cha kuathiri ukuaji
wa pato la taifa na ustawi wa uchumi wetu.
Mbali ya
kuitaka Serikali, kupitia Ikulu kuingilia kati mzozo huu wa sasa, pia kupitia
taarifa hii tunaitaka ifanyie kazi madai yote ya wadau mbalimbali katika sekta ya
biashara ambayo yamekuwepo kwa muda mrefu sasa na CHADEMA kama chama kikuu cha
upinzani, kupitia Kambi ya Upinzani Bungeni imekuwa ikiyasema mara kwa mara,
kupitia kwenye hotuba za Waziri Kivuli au hoja za wabunge wake.
Tunasema
hivyo kwa sababu mgogoro huu wa mashine za EFD ni dalili tu ya tatizo au
matatizo ya msingi ambayo hayatafutiwi majawabu ya kudumu. Ni wajibu wa
Serikali kuhakikisha kuwa nchi hii inatoa fursa nzuri kwa ajili ya watu wake
kuzalisha na kufanya biashara yenye tija kwa wauzaji na wanunuzi kwa ajili ya
uchumi wa taifa na mtu mmoja mmoja.
Imetolewa leo Februari 12, Dar es
Salaam na;
Hyness Kiwia (MB)
Waziri Kivuli wa Viwanda na Biashara
0 comments:
Post a Comment