PICHA
ya mwisho ya Kiongozi wa zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela akiwa hai
imetolewa akionekana mwenye tabasamu huku ameshika mkono wa kitukuu chake.
Picha
hiyo ilipigwa Mei nyumbani kwake Houghton jijini Johannesburg akiwa amekaa
kwenye kiti alichokipenda sana –mwezi mmoja kabla hajalazwa hospitalini jijini
humo.
Kwa
familia ya Mandela picha hiyo inabaki kuwa kumbukumbu nzuri za nyakati za
furaha. Na kwa mtoto wa miaka mitatu, Lewanika, ambaye anaonekana kwenye picha
hiyo, itakuwa ni kumbukumbu ya aina yake, anasema baba yake, aliyeipiga,
akiongeza kuwa kitakuwa ni kitu ambacho ni hazina kwake atakapokuwa amekua
kiasi cha kuweza kuelewa mambo.
Ni
taswira ya mwisho ya mtu wa kihistoria ambaye Waafrika Kusini na walimwengu
duniani wanamwomboleza-huku pia wakisherehekea urithi aliowaachia wa amani, mtu
mashuhuri ambaye karama zake zitahisiwa na kila mtu duniani hata katika miaka
ijayo.
Picha
hiyo inamwonesha Lewanika akiwa amekaa kwenye mkono wa kiti, huku akimwangalia
kwa udadisi mkubwa babu yake, mtu ambaye amekuja kuwa alama ya nchi yake,
katika mapambano dhidi ya maovu, lakini ambaye pia mtoto huyo alizoea kumwita
‘baba’.
Akihojiwa
jana na The Mail on Sunday la Uingereza, baba yake Lewanika, Ndaba
Mandela-ambaye ni mjukuu wa Mandela-alisema alipiga picha hiyo akiamini kuwa
huenda ikawa ni fursa yake ya mwisho kuwapiga picha wawili hao wakiwa pamoja.
“Ilikuwa
Mei, Jumamosi moja mchana. Tulikuwa tumekuja kumjulia hali mzee huyo na
tukamkuta akiangalia kipindi cha National Geographic kwenye televisheni, “Ndaba
(30) alisema.
“Alimwangalia
Lewanika na kumwita, “njoo, njoo.” Uso wa mzee ulijawa nuru alipomwona-kama
ujuavyo alipenda sana watoto. Walikumbatiana na mwanangu akamwita “baba”.
Ilinigusa sana kuwaona wawili hao wakiwa pamoja.”
Ndaba
ambaye ni Mwenyekiti wa Wakfu wa Africa Rising ambayo inashughulikia maendeleo
ya uchumi wa vijana wa Afrika Kusini, anaishi katika nyumba ya Mandela ya
Houghton, ambako ndiko mzee huyo alifia Alhamisi.
Ndaba
alisema: “Tunajivuna kwamba tumeweza kutunza kumbukumbu hii maalumu na kupata
heshima ya kuionesha dunia.”
Alipenda watoto
Binti
wa Mandela, Zindzi (53) naye aliiambia The Mail on Sunday mapema mwaka huu
jinsi baba yake alivyopenda kuwa na watoto na vijana karibu naye. Anakumbuka
simulizi ya jinsi alivyotoka gerezani, alipomwomba aache kumnyonyesha mwanawe
wa kiume ili akae na mtoto huyo chumbani kwake, amlishe na kumlea kila usiku.
Zindzi
alisema wakati fulani:”Baba hufurahi sana anapoona watoto wamemzunguka.
Anawapenda na hufurahi wakimpandapanda.”
Picha
hii ilitoka wakati Mandela akisumbuliwa na maambukizi sugu ya mapafu
yaliyogundulika akiwa gerezani alipotengwa na kuwekwa kwa miezi kadhaa akiwa
ndani ya rumande yenye giza.
Hali
yake ilibadilika ghafla mapema wiki jana, wakati binti yake mkubwa Makaziwe,
aliyezaliwa katika ndoa yake ya kwanza, aliposimulia uchungu wake alipomwona
baba yake akiwa “katika kitanda chake cha mauti.”
Jana
Ndaba, akiwa mwana familia wa kwanza kuzungumza tangu Mandela afariki dunia,
alielezea masikitiko yake makubwa, lakini akaongeza:”Kuna hisia za faraja pia,
kwamba hatimaye yuko mahali pema zaidi. Ni faraja kutambua kuwa mamilioni kwa
mamilioni ya watu duniani wako nasi katika majonzi haya. Nimeona maua yote nje
ya nyumba, haiaminiki.”
Kuhusu
picha hiyo, Ndaba aliongeza: “Siku moja nitamwambia mwanangu Lewanika juu ya
babu yake huyu alivyokuwa maarufu na picha hii itakuwa maalumu kwake.”
Alikumbuka,
kwamba Mandela alikuwa amekaa kwenye kiti chake katika chumba cha kupumzika
nyumbani kwake, huku amezingirwa na vitabu na picha alizopewa kama zawadi,
alipompeleka mwanawe huyo.
Kuna
wakati madaktari walikuwa na wasiwasi na afya yake hasa kutokana na moyo wake
kuzidi kudhoofu; mikono yake iliyovimba kutokana na tatizo hilo, vyote
vinaonekana kwenye picha hiyo.
Baada
ya wiki kadhaa alizidiwa usiku wa manane na kukimbizwa katika hospitali ya moyo
jijini Pretoria ambako alilazwa kwa miezi mitatu. Katika picha hiyo Mandela
anaonekana mwenye furaha kwa kuwa na kitukuu chake.
“Alipozaliwa
nilimwuliza mzee tumwite jina gani,” Ndaba anakumbuka. “Na babu yangu
akapendekeza jina la Ngubencuka ambalo ni la mmoja wa wahenga wetu. Nalazimika
kusema nilikuwa tayari nina jina la Lewanika lakini tukampa jina la katikati la
Ngubencuka.”
Ndaba
alikuwa Brazil akiwakilisha nchi yake katika kura za ratiba ya fainali za soka
Kombe la Dunia aliposikia taarifa za kifo cha babu yake. “Ndio nilikuwa
nimewasili katika eneo la shughuli mara nikapigiwa simu na shangazi. Tulirudi
nyumbani mara moja.”
Alisema
takribani asilimia 90 ya familia tulikusanyika nyumbani kwa Mandela katika
barabara inayopambwa na miti ya mijakaranda katika kitongoji cha watu matajiri.
“Ni
majonzi lakini kila mmoja alikuwa akijishughulisha kulisha ndugu na kuandaa
mambo mbalimbali. Tulikuwa na chakula cha pamoja leo (jana) jambo ambalo ni
jema.”
Miongoni
mwa watu walioshinda nyumbani hapo ni mke wa pili wa Mandela, Winnie. Mke wa
tatu Graca Machel alikuwa pembeni mwa kitanda wakati anakata roho Alhamisi,
pamoja na wajukuu wake kadhaa na wazee wa kimila wa jamii ya Waxhosa.
Walijumuika pia na Mchungaji ambaye alifanya maombi ya mwisho kwa mzee.
Mandela
alikuwa na watoto sita, watatu walishatangulia mbele za haki. Mmoja alikuwa ni
wa kiume Makgatho Lewanika Mandela, ambaye alifariki dunia kwa Ukimwi mwaka
2005 akiwa na umri wa miaka 55. Mjukuu wa Makgatho-aliye na Mandela kwenye
picha hiyo- alipewa jina la kati la babu yake huyo.
Kwa
jumla kuna wajukuu 17 na vitukuu 13. Zenani ambaye ni binti wa mjukuu wa
Mandela, Zoleka, alifariki dunia katika ajali ya gari siku ya mkesha wa
uzinduzi wa sherehe za fainali za Kombe la Dunia mwaka 2010 zilizofanyika
Afrika Kusini. Alikuwa na umri wa miaka 13.
Ndaba
alisema: “Sisi ni familia kubwa na tutakuwa hapa kwa siku chache zijazo. Tukio
kubwa litakuwa ni sherehe za kumbukumbu ya Mandela Jumanne. Kwa maziko ya
Jumapili, nina uhakika kutakuwa na wakuu kadhaa wa serikali za dunia.
“Najua
Obama (Barack-Rais wa Marekani) alisema anataka kuja na Rais wa Ufaransa
anataka kuja pia, na viongozi mbalimbali wa Afrika. Sijasikia ni nani anakuja
kutoka Uingereza”.
Hata
hivyo, habari kutoka Uingereza zilisema Malkia Elizabeth II hatahudhuria maziko
ya Mandela kutokana na ushauri wa madaktari apunguze safari ndefu kutokana na
afya yake. Mwanawe, Prince Charles atamwakilisha.
Malkia
badala yake anatarajiwa kutoa heshima zake katika Misa maalumu itakayofanyika
kwenye Kanisa la Westminster Abbey, London, Uingereza.








0 comments:
Post a Comment