
DAKIKA
za mwisho za maisha yake, Rais mstaafu wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, hakuwa
akitumia mashine ya kumsaidia kupumua.
Mmoja
wa wanafamilia wa Mandela, Bantu Holomisa, aliyemuona kiongozi huyo dakika 90
kabla ya kifo chake, ameripotiwa akisema alikuwa akipumua bila msaada wa
mashine hiyo na alikuwa amezungukwa na wanafamilia wa karibu.
"Wakati anafariki Alhamisi iliyopita
usiku, hakuwa akitumia msaada wa mashine kupumua, alikuwa akipumua bila mashine
hiyo,” alisisitiza mtoa taarifa aliyenukuliwa na gazeti la kila wiki la Sunday
Times.
Mandela
aliyekuwa akisumbuliwa na mapafu, amekuwa akilazwa mara kwa mara kutokana na
matatizo hayo na ni mara chache alikuwa akilazimika kutumia mashine ya
kumsaidia kupumua.
Kwa
mujibu wa gazeti la Sunday Times, Mjukuu wa Mandela, Mandla aliitwa kwa dharura
kutoka katika kijiji alikozaliwa Mandela, Mvezo ili awe karibu na babu yake na
alibaki hapo mpaka alipovuta pumzi ya mwisho.
Mbali
na Mandla, wengine waliokuwepo wakati akikata roho ni viongozi waandamizi wa
chama cha ANC na viongozi wa dini waliokuwa wakijitahidi kufariji familia na
marafiki wa karibu.
Kwa
mujibu wa jarida la kila wiki la City Press, wanafamilia wa karibu waliruhusiwa
kuingia katika chumba cha Mandela wawili au watatu kwa ajili ya kuonana naye
kwa mara ya mwisho.
"Waliokuwa nyumbani wamezungumzia huzuni
kubwa iliyokuwa katika nyumba hiyo,” City Press liliandika.
Ilielezwa
pia kwamba Mandela alikuwa hajaweza kuzungumza neno kwa miezi kadhaa.
Gazeti
la Sunday lilimnukuu Bantu Holomisa, ambaye ni mmoja wa watu waliomuona Mandela
katika dakika za mwisho, akisema alipokea simu akielezwa kuwa hali ya kiongozi
huyo ilikuwa mbaya.
"Nilikwenda moja kwa moja kumuona katika
chumba chake, Nilihuzunika kumuona katika hali ile kwa kuwa alikuwa amebadilika
tangu nilipomuona mara ya mwisho,“ alisema.
Holomisa alisema alikaa kwa zaidi ya saa moja
na Mandela na kuondoka nyumbani hapo dakika 90 kabla ya kifo chake kutokea.
"Familia
ilikuwa inajitahidi kuvumilia na kulikuwa na utulivu. Hali ilikuwa ngumu pale
wanajeshi walipowasili kuchukua mwili wa Madiba karibu saa sita za usiku,”
gazeti hilo lilimnukuu mmoja wa wanafamilia aliyekuwepo.
"Wanajeshi
walipokuwa wakishuka ghorofani katika chumba cha Mandela na mwili wa Madiba
usio na uhai, wakisindikizwa na Mandla,
ndio nilianza kuamini kwamba Madiba hayupo na sisi.”
CHANZO: HABARILEO








0 comments:
Post a Comment