Friday, November 15, 2013

WANACHAMA BIMA YA AFYA WAFIKIA 500,000

 
IDADI ya wanachama wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) imeongezeka kutoka 164,708 hadi kufikia  536,829 kati ya Julai 2012 na Juni 2013.
Mkurugenzi wa Takwimu na Uhai wa wanachama wa Mfuko huo, Michael Mhando aliueleza Mkutano wa wadau wa NHIF na CHF mjini hapa juzi kuwa ongezeko hilo ni sawa na asilimia 69.3.
Aidha, Mhando  alisema idadi ya wanufaika imeongezeka kutoka 691,774 hadi kufikia 2,963,296 kwa kipindi hicho hicho.

Taarifa ya utekelezaji wa shughuli kuu za mfuko huo  hadi kufikia Juni mwaka huu  inaonesha Sh milioni 202 zikiwa ni michango ya wanachama zilikusanywa ikilinganishwa na Sh milioni 11.3 zilizokusanywa Julai 2002 mfuko huo ulipoanzishwa.
 Mhando alisema ili kumudu gharama za shughuli za uendeshaji, mfuko umekuwa ukiwekeza ziada ya fedha kwenye vitega uchumi vya muda mfupi kama vile amana za Serikali, za benki na hisa.
“Mfuko unaruhusiwa kisheria kuwekeza ziada baada ya kutoa fedha za madai, shughuli za uendeshaji wa Mfuko na gharama za maendeleo ya Mfuko” aliwafahamisha washiriki wa Mkutano huo.
Kutokana na uwekezaji huo, alisema, zaidi ya Sh milioni 55.8 zilizalishwa hadi kufikia Juni mwaka huu ikilinganishwa na Sh milioni 38 zilizopatikana mwaka jana.
“Fedha za uwekezaji zimeendelea kuwa chanzo muhimu kwa mfuko kuendesha shughuli mbalimbali wakati michango ya wanachama inatumika kulipia huduma za matibabu,” alisema.
Mkurugenzi huyo alisema mfuko unagharimia matibabu yote kwa wanachama wake isipokuwa upasuaji wa urembo, gharama ya tiba kwa madhara ya ulevi au dawa za kulevya na za tiba kutokana na madhara ya kutaka kujiua au kujinyonga.

 Alitaja changamoto zinazoukabili mfuko ni pamoja na kutopatikana huduma zote ambazo mfuko unazitoa katika baadhi ya vituo vyenye hadhi ya kutoa huduma hizo.

Pia upo upungufu wa dawa na baadhi ya wanachama na watoa huduma kutokuwa waaminifu.

Wilaya ya Chemba yaanza kuunda vikundi vya vijana

0 comments:

Post a Comment