Thursday, November 28, 2013

ICC YATENGUA UAMUZI WAKE SASA YATAKA RAIS KENYATTA KUHUDHURIA MAHAKAMANI

MAHAKAMA  ya Kimataifa ya kushughulikia kesi za uhalifu wa kivita, ICC imetengua uamuzi wake wa awali uliomruhusu Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta kutohudhuria baadhi ya vikao vya kesi ya uhalifu wa kivita inayomkabili.

Mahakama hiyo sasa imesema kuwa ni lazima Rais Kenyatta afike mbele ya mahakama hiyo kusikiliza kesi yake na ushahidi unaotolewa dhidi yake.

Mahakama hiyo imesema kama sheria inavyotaka, Rais Kenyatta lazima binafsi ahudhurie vikao vya kesi inayomkabili. Imesema maombi yoyote ya baadaye ya kutaka asihudhurie baadhi ya vikao vya kesi hiyo, yatafikiriwa kutokana na msingi wa suala linaloombewa ruhusa hiyo.

Mahakama hiyo imefikia uamuzi kwamba hukumu iliyotolewa katika rufaa ya tarehe 25 Oktoba 2013 ya Mwendesha mashitaka dhidi ya William Samoei Ruto na Joshua Arap Sang, imetoa taarifa mpya muhimu ambayo inahalalisha kuangaliwa upya kwa suala la kesi hiyo.

Mahakama ya Rufaa ya ICC imehitimisha kuwa Mahakama ina hiyari kwa mujibu wa kifungu namba 63(1), kinachosema kuwa "mtuhumiwa ni lazima awepo mahakamani wakati kesi inayomkabili ikiendeshwa", lakini hiyari hiyo imewekewa kikomo.

 Mahakama ya Rufaa imetoa uamuzi kwamba mtuhumiwa kutofika mahakamani, inaruhusiwa pale tu panapokuwa na sababu maalum na za kipekee, na lazima sababu hizo ziwe zinakidhi hoja kwa mtuhumiwa kutofika mahakamani hapo.

Imeendelea kusema kwamba uamuzi wa kama mtuhumiwa aruhusiwe kutohudhuria sehemu ya vikao vya kesi yake lazima uzingatie hali halisi ya ombi la mtuhumiwa.

Awali mahakama hiyo ya ICC katika uamuzi wake wa tarehe18 October 2013, ilitoa masharti kwa upande wa utetezi wa Bwana Uhuru Muigai Kenyatta kuwepo mahakamani hapo wakati wa ufunguzi na kufunga kesi inayomkabili badala ya kuwepo wakati wote. Wakati huo angeweza kusikiliza maelezo kutoka pande zote na kusikiliza maoni ya waathirika wa ghasia za baada ya uchaguzi mkuu wa 2007 nchini Kenya. Pia angetakiwa kuwepo siku ya kufunga kesi hiyo kwa kusikiliza hukumu yake.
SOMA ZAIDI: BBC SWAHILI

0 comments:

Post a Comment