Tuesday, September 17, 2013

Platinum Credit Ltd Yakabidhi Vifaa vya MIchezo ya Shimiwi

Na Benedict Liwenga-MAELEZO-Dar es Salaam.

KAMPUNI inayojishughulisha na utoaji wa mikopo kwa watumishi wa Serikali na kampuni zilizothibitishwa ijulikanayo kama Platinum Credit Ltd leo imekabidhi vifaa vya michezo kwa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Jeshi la Magereza na TAMISEMI kwa ajili ya maandalizi ya michezo ya Shimiwi inayotarajiwa kuanza hivi karibuni mjini Dodoma.

Akikabidhi vifaa hivyo Mkurugenzi wa Fedha wa Kampuni hiyo Bw. Elias Samwel amesema kuwa kampuni yake inajihusisha na utoaji wa mikopo ya fedha kwa watumishi wa serikali na kampuni zilizothibitishwa na kiasi cha ziada wanachokipata wanakitumia katika kusaidia jamii katika shughuli mbalimbali ikiwemo michezo.

Aidha, kampuni hiyo imekabidhi jezi, tisheti na kofia zenye thamani ya shilingi milioni 10 ili ziweze kusaidia katika michezo ya Shimiwi itakayofanyika hivi karibuni mjini Dodoma.

“Thamani ya vifaa hivi ni ndogo lakini ninaamini kuwa vitasaidia katika kuleta chachu ya maendeleo katika michezo ya shimiwi”. Alisema Samwel. Kwa upande wake Katibu wa Klabu ya Michezo Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Bw. Saidi Marusu ameishukuru kampuni ya Platinum Credit Ltd kwa mchango wao mkubwa waliojitolea katika kusaidia kutoa vifaa vya michezo.

“Kwa niaba ya Wizara Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo napenda kutoa shukurani kwa kupokea vifaa hivi kwani ninaamini kuwa vitaleta chachu katika mashindano haya ya Shimiwi”. Alisema Bw. Marusu.

Naye Kamishna Msaidizi wa Jeshi la Magereza Mkwanda Hassid Mkwanda ameishukuru kampuni hiyo kwa kupata vifaa hivyo na amesema kuwa vitasaidia kwa kiasi kikubwa kufanikisha malengo yao katika michezo ya Shimiwi. “Vifaa hivi vitatumika kwa lengo lililokusudiwa na sio vinginevyo”. Alisema Mkwanda.

Naye mwakilishi wa TAMISEMI ambaye ni Katibu Mkuu wa Shimiwi Bw. Ramadhani Sululu ameishukuru kampuni hiyo kwa mchango wake mkubwa wa kutoa vifaa hivyo vya michezo na ameongeza kuwa vifaa hivyo vitasaidia kuleta hamasa katika michezo.

“Katika mashindano ya Shimiwi tumejiandaa vizuri na tunaamini kuwa tutashiriki vema katika michezo hiyo”. Alisema Sululu. Mashindano ya Shimiwi yanahusisha Wizara zote za Serikali na Taasisi zake ambapo itajumuisha michezo ya kuvuta kamba, mpira wa miguu, pete, riadha, drafti, bao, karata na kurusha tufe.

0 comments:

Post a Comment