Thursday, June 13, 2013

Orijino Komedi Waula

KUNDI la Uigizaji la Orijino Komedi limeingia mkataba wa miaka mitano na Kampuni ya Nexus Consulting Agency na Rockstar 4000 ya Afrika Kusini ambao utawezesha kazi zao kuonekana nje ya Tanzania.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mkataba huo jijini Dar es Salaam jana, Kiongozi wa Orijino Komedi, Seki David alisema mkataba huo umewapa maslahi mazuri wasanii wa kikundi hicho na kuwawezesha kufanya kazi zao kitaalamu.

Hata hivyo, alikataa kutaja kiasi cha fedha walichopata kwa kuingia mkataba huo.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mwakilishi wa Rockstar 4000, Christine Mosha alisema Kampuni ya Nexus imenunua haki zote za usimamizi wa biashara na uongozi wa kundi hilo, lengo likiwa ni kuboresha kazi zao na kuwatafutia masoko nje ya nchi.

Mosha alisema wanakusudia kuzifanya kazi za kundi hilo ambalo linaonesha vichekesho vyake kupitia televisheni ya TBC1 kuonekana katika nchi nyingine za Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla.

Aliainisha majukumu yake kuwa ni pamoja na uboreshaji na uandaaji wa vipindi vya Orijino Komedi pamoja na kukuza vipaji vya wasanii hao kupitia kazi zao nyingine wanazozifanya.

Alisema wanakusudia kurusha vipindi hivyo katika televisheni mbalimbali barani Afrika, na kwa kuanzia wataweka vichwa vidogo vya habari vya lugha za Kiingereza na Kifaransa na hatimaye kuwawezesha kutengeneza programu zao kwa Kiingereza.

Aidha, alisema ndani ya mkataba huo, wasanii wa Orijino Komedi watapata nafasi ya kufanya kazi na wasanii wakubwa Afrika na nje ya Bara la Afrika ambao wana mikataba ya kazi na Rockstar 4000.

Wakizungumza na waandishi wa habari baada ya mkataba huo, wasanii wa Orijino Komedi wameelezea kuridhishwa na mkataba huo ambao pamoja na mambo mengine, unalenga kuendeleza vipaji vya wasanii hao ili vifikie kiwango cha juu cha ufanisi ndani ya Afrika na kimataifa kwa jumla.

0 comments:

Post a Comment