Wednesday, February 12, 2014

Serikali yapongeza Tamasha la Krismasi

 SERIKALI kupitia Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) imeipongeza Kampuni ya Msama Promotions kufanikisha tamasha jipya la Krismasi lililofanyika mwishoni mwa mwaka jana. Licha ya kampuni hiyo kupitia Kamati ya Maandalizi kukumbana na changamoto mbalimbali, Basata limeipongeza kampuni hiyo  kwa kuanza vema katika mikoa mitano lilikofanyika.

Akizungumza katika Kikao cha kuwasilisha ripoti ya tathmini ya Tamasha la Krismasi iliyofanyika jana kwenye ukumbi wa mikutano wa Basata, Ofisa Sanaa  wa Basata, Rajabu Zubwa alipongeza licha ya kwamba imekumbana na changamoto ikiwa pamoja na kulipeleka mkoa wa Tanga ambao una idadi kubwa ya waislamu ni wengi.

Zubwa pamoja na kupongeza alitoa mapendekezo yatakayopunguza gharama katika tamasha hilo na ili kufanikisha gharama ambazo zitawafikia walengwa ambao ni wenye uhitaji maalum, Kamati hiyo inatakiwa kupunguza  waimbaji kutoka nje  kwa kuwa viingilio ni vidogo. “Mnapoandaa tamasha jaribuni kutulia sehemu moja kwa ajili ya kukwepa hasara pia punguzeni idadi ya watu ni kubwa, gharama haiwezi kurudi,” alisema Zubwa.

Naye Ofisa Sanaa Mkuu, Philemon Mwasanga alipongeza Msama kuandaa tamasha hilo na kueleza lilikuwa zuri  na aliishauri Kamati kuwa makini na ualikaji wa waimbaji kutoka nje ya nchi kwa kuwa wengi  wamekuwa wakifanya kinyume  na maadili ya ufikishaji wa Neno la Mungu  kwa njia ya uimbaji.

Alisema waimbaji  wengi wa sasa wamemuweka Yesu nyuma hawana tofauti na wanamuziki wa Bongo Fleva huku akitaka ziwekwe sheria za tamasha kwa waimbaji hao zitakazodhibiti mambo mbalimbali  ikiwemo mavazi, nidhamu  na mengineyo.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Tamasha hilo, Abihudi Mang’era alisema wamekumbana na changamoto nyingi ikiwa pamoja na kutopata wahudhuriaji wengi katika mkoa wa Tanga.  

Mang’era alisema changamoto nyingine ni viingilio vidogo hasa ukizingatia hakuna wadhamini kabisa na alitumia fursa hiyo kuwaomba Basata kuliona hilo na kuwasaidia katika matamasha yake yajayo.    

0 comments:

Post a Comment