Saturday, February 8, 2014

Abakwa na genge la wanaume kwa amri ya ‘mahakama’

POLISI katika eneo la West Bangal nchini India inawashikilia watu 13 wanaodaiwa kumbaka mwanamke kwa amri ya viongozi wa kijiji ambao walimkatalia kuwa na uhusiano na mwanaume aliyetaka kuolewa naye.
Mwanamke huyo wa miaka 20 amelazwa katika hospitali moja akiwa anapata matibabu huku hali yake ikielezwa kuwa mbaya.
Mahakama zisizo rasmi katika vijiji nchini India mara nyingi hupitisha maamuzi ya kuuawa kwa wapenzi wanaodhaniwa kuvunja maadili katika eneo husika.
Vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia vinazidi kuongezeka nchini India tangu tukio la genge la wanaume mwaka 2012 kumbaka na kumwua mwanafunzi katika basi moja jijini Delhi.
Serikali imeimarisha sheria za kudhibiti vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia mwaka jana baada ya maandamano makubwa yaliyosambaa maeneo mbalimbali kupinga tukio hilo dhidi ya mwanafunzi huyo.
Lakini vitendo vya kikatili na ubaguzi dhidi ya wanawake bado vipo kwa wingi nchini India kutokana na mfumo dume wenye kuota mizizi katika jamii nchini humo.
Polisi wanasema tukio hilo la hivi karibuni kabisa lililotokea Jumatatu usiku lilisababishwa na uhusiano wa kimapenzi kati ya mwanamke ambaye ni kabila tofauti na mwanaume aliyekuwa na uhusiano naye.
“Uhusiano wa wapenzi hao wawili ulikuwa unaendelea kwa karibu miaka mitano. Wakati mwanaume mhusika alipomtembelea mwanamke huyo Jumatatu na kupendekeza kumwoa, wanakijiji walimwona na kupanga kumpeleka
katika mahakama ya kijiji.
Wakati wa kusikilizwa kwa kesi hiyo wapenzi hao wawili walikuwa wamefungwa mikono yao,’’ Mkuu wa Polisi wa Birbhum C Sudhakar aliliambia Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC).
Alisema kiongozi wa kijiji hicho aliamuru wapenzi hao kulipa faini kiasi cha Rupia 25,000 (sawa na dola 400) kwa kosa la ‘kuwa wapenzi’.
Mwanaume alilipa faini lakini mwanamke alishindwa kulipa, polisi ilisema.
Kiongozi huyo wa kijiji ambaye inasemekana kuwa ni ndugu wa mbali wa mwanamke huyo anadaiwa aliamuru kubakwa kwa mwanamke huyo, alisimulia afisa huyo wa polisi.

0 comments:

Post a Comment