Wednesday, December 18, 2013

Soma kwa undani jinsi ndege ya Ethiopia Airlines ilivyonusurika kuua watu






Na  Veronica Mheta, Arusha

NDEGE ya Shirika la Ndege la Ethiopia,  imetua kwa dharura katika uwanja mdogo wa Arusha baada ya kushindwa kutua katika uwanja wa Kimataifa wa Kilimanjaro
(KIA) kutokana na ndege nyingine ya TFC kukwama kwenye njia ya kurukia.

Aidha, ndege hiyo ya Ethiopia aina ya Boeing 767 namba ET- AQW iliyokuwa ikitoka Ethiopia ili kutua KIA na iliwasiliana na waongoza ndege wa KIA waliotoa maelekezo ya kutua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta, lakini rubani huyo alishindwa kufika Nairobi na kulazimika kutafuta uwanja mwingine wa karibu ndipo alipotua uwanja mdogo wa Arusha.

Hata hivyo, ndege hiyo iliyotua saa 6 mchana uwanjani hapo, ilititia kwenye tope wakati rubani akijaribu kukata kona katika uwanja huo mdogo ambao hauruhusu kutua ndege kubwa.

Hali hiyo ilizua taharuki kwa wafanyakazi wa kiwanja hicho na abiria waliokuwa wakisubiri ndege zingine  kwenda sehemu mbalimbali  za utalii na safari za kawaida.

Baada ya kutua salama, abiria wa ndege hiyo zaidi ya 213 na wafanyakazi  23 waligoma kushuka kwa kutumia ngazi za kiwanjani hapo na kukaa ndani ya ndege kwa karibu saa tano wakisubiri ngazi kubwa kutoka KIA.

Kugoma kushuka kwenye ndege hiyo kulisababisha baadhi ya wafanyakazi wa ndege hiyo kufungua milango ya dharura ili abiria wapate hewa.

Kwa  mujibu wa wafanyakazi wa uwanja huo wa Arusha, ndege hiyo ililazimika kutua hapo kutokana na kuishiwa mafuta.

Mmoja wa mashuhuda hao ambaye hakutaka jina lake liandike gazetini kwa madai ya kuwa si msemaji, alisema haijawahi kutokea ndege kubwa kama hiyo kutua uwanjani hapo salama, lakini kwa kuwa ni kubwa ilikwama kwenye tope na kusababisha hofu kubwa ila vyombo vya usalama vilikuwapo.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo ambaye alifika eneo la tukio alisema tukio hilo halijapata kutokea lakini akasisitiza kuwa kuna haja ya kuboresha uwanja huo  ili hata zinapotokea dharura zishughulikiwe kwa wakati.
SOMA ZAIDI: HABARILEO ONLINE

0 comments:

Post a Comment