Thursday, November 21, 2013

TSNP, UDHRA WAMTAKA WAZIRI MKUU ATOE RIPOTI YA MATOKEO MABAYA YA KIDATO CHA NNE

MTANDAO wa Wanafunzi nchini(TSNP) na Jumuiya ya Kutetea Haki za Binadamu ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam(UDHRA) wamemtaka Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuweka hadharani ripoti ya Tume ya kuchunguza matokeo ya kidato cha nne mwaka jana ndani ya wiki moja.
Mkurugenzi wa TSNP, Alphonce Lusako alisema jana kuwa pamoja na juhudi zinazofanywa na serikali katika kuimarisha elimu lakini bado kuna changamoto kubwa katika ukuaji wa sekta ya elimu.
“Kwa niaba ya watanzania na wadau wa elimu waliowengi tunasikitishwa na usiri wa tume ya kuchunguza matokeo ya kidato cha nne iliyoundwa na waziri Mkuu mwaka huu” alisema.
Alisema “tunamtaka waziri mkuu ndani ya wiki moja atoe ripoti ya Tume hadharani juu ya madhaifu yaliyopatikana, wakina nani wamehusika na madhaifu husika, mapendekezo ya tume husika ili yasijirudie tena kwa wadogo zetu wa kidato cha nne, wanaofanya mtihani sasa”.
Lusako alisema “ikumbukwe kwamba kwa sasa kidato cha nne wapo kwenye miihani yao ya mwisho lakini bado tume iliyoundwa kwa ajili ya kuchunguza madhaifu ya mitihani ya kidato cha nne mwaka uliopita bado imekuwa ni siri ya tume na waziri mkuu”.
Alisema endapo waziri mkuu hatatoa ripoti yake ndani ya wiki moja watachukua jukumu la kuwaunganisha wanafunzi wa vyuo vikuu nchini, wanafunzi wa sekondari na shule za msingi nchini, asasi zisizo za serikali, wadau mbalimbali wa elimu, vyama vya siasa, wazazi na watanzania kwa ujumla wake ambao wameunga mkono umahututi wa mfumo wa elimu kufanya maamuzi ili kunusuu elimu nchini.
Aliwaomba watanzania wote kushirikiana kwa suala hilo kwa kuwa suala la elimu ni la watanzania wote na si la serikali pekee na kusisitiza kamba elimu itabadilishwa na watanzania na itauawa na watanzania.
Mwisho


0 comments:

Post a Comment