Saturday, November 9, 2013

Afa safarini kwa kupasukiwa dawa za kulevya alizomeza


KIJANA mmoja amefariki dunia baada ya kubainika kuwa moja kati ya kete za dawa za kulevya alizokuwa akisafirisha kwa kuzimeza tumboni kupasuka.
Kijana huyo ambaye hajafahamika ni mkazi wa wapi amekutwa na kete 65 za dawa zinazosadikiwa kuwa za kulevya na alikuwa akitokea Dar es salaam kwenda Lilongwe nchini Malawi kwa basi mali ya kampuni ya Taqwa lenye namba  T 319 BLZ aina ya Nissan.
Kamanda wa Polisi mkoani Mbeya, Diwani Athumani alisema kwa mujibu wa hati ya kusafiria kijana huyo amefahamika kwa jina la Kassim Said Mboya(36), lakini jina lililokuwa kwenye tiketi yake ya basi hilo ni Kassim Mueck Michael.
Kamanda Athuman aliwaambia waandishi wa habari kuwa juzi(Novemba 7) majira ya asubuhi basi alilokuwa akisafiria kijana Kassim lilifika Kasumulu mpakani mwa Tanzania na Malawi na abiria wote kutakiwa kushuka kwa ajili ya kushughulikia taratibu za kuvuka mpaka kama ilivyozoeleka.
Tofauti na abiria wenzake, kijana huyo alibaki ndani ya gari huku hali yake ya afya ikionekana kudhoofu na ndipo wafanyakazi wa basi hilo walipochukua uamuzi wa kutoa taarifa kituo cha polisi kilichopo jirani na kisha askari wa jeshi hilo kumchukua na kumpeleka katika hospitali ya wilaya ya Kyela.
Alisema kutokana na kudhoofu kwake na dalili  alizokuwa nazo ilibidi polisi washauriane na maadaktari na ndipo yakachukuliwa maamuzi ya kumfanyia uchunguzi wa miale(X Ray) na kubaini kuwa tumboni mwake kulikuwa na vitu aina ya pipi na kuwa huenda ndivyo vilimfanya adhoofu kiasi hicho.
Alisema kwa bahati mbaya wakati huo wote hali ya kijana Kassim iliendelea kuwa mbaya na hatimaye kufariki dunia wakati uchunguzi huo ukiendelea na ndipo ikalazimu mwili wake kusafirishwa hadi hospitali ya Rufaa Mbeya kwaaajili ya uchunguzi zaidi.
Kamanda huyo alisema baada ya mwili huo kufikishwa hospitali ya rufaa ulifanyiwa uchunguzi kwa kupasuliwa na ndipo walipokuta kete 65 za dawa hizo zinazosadikiwa kuwa za kulevya huku moja kati ya hizo ikionekana kutoboka hali iliyoleta hisia kuwa ndiyo iliyosababisha kijana huyo kupoteza maisha.
“Kijana huyu pia alikuwa na begi dogo lenye suruali moja aina ya jeans, fulana moja nyeusi,raba jozi moja rangi nyekundu,mkate mmoja,mkoba mdogo wa kiunoni, kadi mbili za kinga ya ugonjwa wa manjano,randi mbili sarafu za Afrika kusini na mifuko sita ya Rambo ya rangi nyeusi” alisema
Kamanda Athuman alisema taratibu zinafanyika ili dawa hizo zipelekwe ofisi ya mkemia mkuu wa serikali kwa uchunguzi wa kitaalamu ikiwa ni pamoja na kujua aina ya dawa na uzito wake.
Aliwataka wakazi mkoani hapa kufika katika chumba cha kuhifadhia maiti katika hospitali ya Rufaa Mbeya kwaajili ya kuutambua mwili wa kijana huyo ambaye hafahamiki ni mkazi wa wapi.

0 comments:

Post a Comment