Sunday, September 15, 2013

Wanaojihusisha na ujangili watakiwa kujisalimisha

Na Lucy Lyatuu

SERIKALI imewataka wafanyabiashara, wanasiasa na watumishi wa umma wanaojihusisha na ujangili, kujisalimisha haraka.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, alisema hayo jana Dar es Salaam mara baada ya kupokea ujumbe wa matembezi ya hiari yaliyoandaliwa na Mfuko wa Hifadhi Wanyamapori (AWT).
Amesema pia Serikali inakusudia kuwafikisha katika vyombo vya Dola watuhumiwa na kuwatangaza kwenye vyombo vya habari ili  umma na dunia ifahamu wahujumu rasilimali hiyo.
Nyalandu alisema Serikali inajenga uwezo wa kukabiliana na majangili porini na matajiri wanaofadhili ujangili ambao wako Dar es Salaam, Morogoro, Arusha, Nairobi (Kenya) na hata Beijing nchini China. 
“Dawa ya majangili imekwishachemka na inapelekwa mezani wakati wowote...ole wake atakayenyweshwa  dawa hiyo,” alisema Nyalandu huku akitoa onyo kwa wanaojihusisha kuacha kabisa uovu huo, vinginevyo watajikuta wamenaswa na vyombo vya Dola.

Alisema ujangili umechangia kupungua idadi ya tembo nchini kutoka 350,000 miaka ya 1960, hadi 110,000 mwaka 2009, huku idadi ya tembo wanaouawa na majangili ikizidi kuongezeka kila mwaka. 

Alitoa mfano wa mwaka 2010 ambao tembo waliouawa walikuwa 259, mwaka 2011 tembo waliouawa walikuwa 276 na mwaka 2012 walikuwa tembo 473 huku kati ya Januari hadi Julai mwaka huu, tembo 378 wakiuawa.

Hata hivyo alisema Serikali imekuwa ikipambana na majangili hao ndani na nje ya hifadhi za taifa, na katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita kuanzia (2010 – 2012),  majangili 4,066 walikamatwa na bunduki 1,899 kukamatwa na kutaifishwa. 

Kuhusu matembezi yaliyoanzia jijini Arusha Agosti 24,2013, aliwapa pole wananchi 18 waliotembea kwa hiyari kutoka Arusha hadi hapa Dar es Salaam na kuongeza kuwa ubunifu huo umebeba ujumbe mkubwa kuhusu kupiga vita ujangili nchini. 

Kwa upande wake muanzilishi wa matembezi hayo, Pratik Patel amewataka Watanzania kuamka na kuhakikisha wanatokomeza ujangili kwani ni rasilimali inayopotea pasipokuwa na manufaa.
Alisema  ametumia siku 19 kutembea bila kulipwa chochote ambapo vuguvugu hilo halitoishia katika matembezi hayo na kwamba atakwenda kuhamasisha wananchi  nyumba kwa nyumba namna ya kuwa walinzi wazuri wa rasilimali zao.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge Ardhi Maliasili na Mazingira, James Lembeli alisema endapo wimbi la ujangili litaachwa liendelee bila ya hatua stahiki kuchukuliwa katika miaka 10 ijayo Tanzania haitokuwa na tembo.

Alisema hata kitendo cha matembezi hayo kimeionesha Serikali kuchukua hatua za haraka kwani tembo wamekuwa wakiingiza mabilioni ya fedha.

Alisema kila mwezi tembo 800 huuawa huku kwa mwaka ikifikia tembo 10,000 jambo ambalo hivi sasa hakuna anayeweza kutoa idadi ya tembo waliobaki.
“Serikali inatakiwa kuchukua hatua za haraka, kwani kipindi cha nyuma lipo gari la Wizara ya Elimu lilikamatwa likiwa na meno ya tembo na mhusika alikamatwa kwa siku tano tuu baada ya hapo akaachiwa huru jambo ambalo linatakiwa kutazamwa upya,” alisema Lembeli.
Mbali na matembezi hayo, Mfuko wa uhifadhi wanyamapori Fredkin Conservation Fund  umekabidhi hundi ya dola za kimarekani milioni 2.25 kwa ajili ya kupambana na ujangili nchini.

0 comments:

Post a Comment