JESHI la Polisi limesema anayedaiwa kuwa muuaji wa
Padri Evarest Mushi amekamatwa na ametambuliwa na watu walioshuhudia tukio
hilo.
Kauli hiyo ya Polisi inakuja siku moja baada ya Askofu
Mkuu wa kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam Mwadhama Polycarp Kardinali
Pengo kulilaumu Jeshi la
Polisi kwa kuzembea kuwakamata watuhumiwa wa mauaji ya padri huyo.
Akizungumza na
waandishi wa habari mjini Zanzibar jana, Kamishna wa Polisi Zanzibar, Mussa A.
Mussa alisema upelelezi wa kesi hiyo ya
mauaji ya Padri Mushi umefikia mahali pazuri.
“Napenda kuwapa taarifa ya maendeleo ya kesi ya
mauaji ya Padri Evarest Mushi. Najua si ninyi tu waandishi wa habari lakini Watanzania
wote wanataka kujua maendeleo ya upelelezi wa tukio hili.
“Jeshi la Polisi liliwaahidi litawajulisha kila
hatua iliyofikiwa juu ya upelelezi wa shauri hili. Mpaka hapa tunapozungumza
upelelezi wa shauri hili umefikia pahala pazuri na jalada la shauri hili
limeshapelekwa kwa Mkurugenzi wa Mashtaka kwa hatua za kisheria.
“Muhusika wa mauaji haya tayari amekamatwa na
ametambuliwa na watu walioshuhudia tukio hilo, “ alisema Kamishna Mussa.
Alisema Jeshi la Polisi lilichukua hatua kadhaa za
kiupelelezi ikiwa ni pamoja na kuchora michoro ya sura ya mtu
kwa kutumia watu walioshuhudia tukio hilo na kwamba baada ya kuitoa picha hiyo
katika vyombo mbalimbali vya kiulinzi, wananchi, vyombo vya habari na mitandao
ya kijamii muhalifu huyo ametambulika.
“Jeshi la Polisi liliahidi kutoa milioni kumi kwa
watu watakaosaidia kupatikana kwa muhalifu huyu. Ahadi ile ipo pale pale na
mwananchi aliyesaidia kutoa utambuzi Jeshi la Polisi litamzawadia kiwango hicho
cha fedha, lakini kwa usalama wa shahidi huyo na kwa sababu za kiupelelezi
tukio la kumkabidhi fedha hizo hatutaliweka bayana katika vyombo vya habari.
“Mwisho kabisa, naomba niwashukuru tena wananchi
wote wa Zanzibar kwa kuwa karibu na ofisi yangu na Jeshi la Polisi kwa ujumla
katika mapambano ya vitendo vya kihalifu,” alisema Kamishna Mussa.
Katika hatua nyingine Kamishna huyo wa Polisi
Zanzibar amewahakikishia amani na utulivu wananchi wa Zanzibara wakati wa
Sikukuu ya Pasaka.
“Napenda kuendelea kuwahakikishia uwepo wa usalama
na amani kwa muda wote wa mapumziko na Ibada za Pasaka.
“Jeshi la Polisi linawahakikishia kuendelea
kudumisha doria za mjini na vijijini kwa kutumia gari, askari wa miguu,
pikipiki na mbwa ili kuhakikisha usalama unadumu visiwani hapa.
“Tutaendelea kutoa ushauri wa kiusalama na
kushirikiana kwa karibu zaidi na wananchi wote kuona maisha na mali zao
zinakuwa salama. Tunawaomba wenye mahoteli ya kitalii na nyumba za starehe kuwa
karibu na Jeshi lao la Polisi pamoja na kufuata ushauri wote wa kiusalama
wanaopewa kila wakati.”
0 comments:
Post a Comment