Friday, October 18, 2013

ZITTO ASHIKA VYAMA PABAYA

MWENYEKITI wa Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC), Kabwe Zitto, ameendelea kusisitiza kuwa hadi sasa hakuna chama chochote cha siasa kilichowasilisha ripoti ya ukaguzi wa hesabu zake kwa Msajili wa Vyama vya Siasa na kuvitaka vyama hivyo kuacha propaganda na kulichukulia suala hilo kisiasa.
Amesema hazungumzi suala hilo kama Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, bali anasimamia Sheria na kama hawataki, wamshauri Spika wa Bunge, Anne Makinda, avunje kamati yake.
“Napenda niwaambie nazungumzia suala hili si kama Naibu Katibu Mkuu wa Chadema bali Mwenyekiti wa PAC na ninasimamia sheria,” alisema.
Akizungumza jana katika ofisi ndogo za Bunge jijini Dar es Salaam, Zitto alisema tangu atoe tamko la kutaka vyama hivyo vijiandae kujieleza kwanini havijawasilisha ripoti hizo za ukaguzi, amekuwa akisikia kelele tu na hakuna chama chochote kilichotekeleza kisheria jukumu hilo la kuwasilisha taarifa zake kwa Msajili tangu 2009 kama vinavyodai.
“Najua kuna vyama vinajitetea kuwa tayari vimefanya ukaguzi wa hesabu zake, sasa kama kweli ziko wapi hizo ripoti, Sheria iko wazi, ukaguzi ukikamilika ripoti inatakiwa kuwasilishwa kwa Mkaguzi Mkuu na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG), na Msajili na si kuzifungia kabatini,” alisisitiza Zitto.
Alisema amemuagiza Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, kuwaandikia barua ya kisheria viongozi wa vyama tisa vinavyopata ruzuku ya Serikali, ya kuwaita mbele ya kamati hiyo, Oktoba 25, mwaka huu ili kujieleza kwanini hawajawasilisha ripoti hizo kwa Msajili kwa kipindi cha miaka minne iliyopita.
Vyama hivyo ambayo vimeshakula Sh bilioni 67.7 bila kutoa ripoti ya matumizi yake ni CCM Sh bilioni 50.9, Chadema Sh bilioni 9.2, CUF bilioni 6.3, NCCR-Mageuzi Sh milioni 677, TLP Sh milioni 217, UDP Sh milioni 333, DP Sh milioni 3.3, APPT-Maendeleo Sh milioni 11 na Chausta Sh milioni 2.4.
SOMA ZAIDI: HABARILEO ONLINE

0 comments:

Post a Comment