Friday, May 3, 2013

ISHA MASHAUZI APANDISHWA KIZIMBANI LEO, AHUSISHWA NA KESI YA WIZI

MWANAMUZIKI mashuhuri wa taarab Isha Ramadhan maarufu kama Isha Mashauzi (25) amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Mwanzo ya Kariakoo akikabiliwa na mashitaka ya wizi.
Isha ambaye ni mkazi wa Kinondoni pamoja na mwenzake Halima Shabani (26) walifikishwa mahakamani hapo jana kusomewa mashitaka yanayowakabili mbele ya Hakimu Matrona Luanda.
Karani Blanka Shayo wa mahakama hiyo, alidai mbele ya Hakimu Luanda kuwa washitakiwa hao walitenda kosa hilo Aprili 20, mwaka huu katika mtaa wa Mafia na Jangwani eneo la Kariakoo.
Shayo alidai kuwa siku ya tukio, washitakiwa wote kwa pamoja waliiba pochi moja ya mkononi iliyokuwa na Sh 758,000 kutoka dukani kwa Sara Peter, mali ya Veronica Taki.
Hata hivyo baada ya kusomewa mashitaka hayo, walikana kutenda kosa hilo na washitakiwa wapo nje kwa dhamana baada ya kukamilisha masharti ya kuwa na mdhamini mmoja kwa kila mshitakiwa aliyetakiwa kusaini hati ya dhamana ya Sh milioni 1.5. Kesi hiyo itatajwa tena Mei 14, mwaka huu.

0 comments:

Post a Comment