ALIYEKUWA mgombea Ubunge wa Jimbo la Ubungo kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika uchaguzi mkuu wa 2010, Hawa Ng’humbi jana ameondoa rufaa ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa mwaka juzi yaliyompa ushindi Mbunge wa Jimbo hilo John Mnyika.
Rufaa hiyo ilitakiwa kuanza
kusikilizwa jana katika Mahakama ya Rufaa Kanda ya Dar Es Salaam mbele ya jopo
la Majaji watatu, Jaji Salum Massati, Jaji Nathalia Kimaro na Jaji Catherine
Urio.
Hata hivyo, Ng’humbi kupitia kwa
Wakili wake Issa Maige aliiomba Mahakama hiyo kuondoa rufaa hiyo kwa madai kuwa
ameshakubaliana na mrufani wake (Mnyika).
Kutokana na ombi hilo la upande
wa mrufaa, Kiongozi wa jopo hilo la Majaji, Jaji Urio alisema Mahakama imefuta
rufaa hiyo.
Ng’humbi alifungua kesi akipinga
matokeo ya uchaguzi mkuu wa mwaka juzi yaliyompa ushindi Mnyika kwa madai
kulikuwa na ukiukwaji wa taratibu, kanuni na sheria za uchaguzi katika uchaguzi
huo.
Mei 24 mwaka huu, Jaji Upendo
Msuya wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaam alitupilia mbali maombi ya
Ngh’umbi na kuthibitisha Mnyika kuwa Mbunge halali wa Jimbo la Ubungo.
Jaji Msuya alisema Ng’humbi
alishindwa kuthibitisha madai yake na kuonesha jinsi yalivyoathiri matokeo ya
uchaguzi huo na kutangaza kuwa uchaguzi huo ulikuwa halali na kumtaka alipe
gharama za uendeshaji wa kesi.
Ng’humbi alikuwa na hoja tano
ambazo ni Mnyika alimtuhumu kuuza nyumba za Umoja wa Wanawake (UWT) , Kutumia
Laptop za Mnyika kuhesabu kura, kuingia watu wengi wa Chadema katika chumba cha
kuhesabia kura, kuwepo kwa kwa kura hewa 16,000 na kukosewa kwa karatasi
za kujumlisha kura (form).
Katika
hukumu hiyo Jaji Msuya alisema, mashahidi wa Ng’humbi hawakuonesha wala
kuthibitisha madai yaliyowasilishwa yalitendeka vipi na ni namna gani
yaliathiri matokeo ya uchaguzi.
Katika
madai kuwa zaidi ya kura 14,000 alizodai hazieleweki zilitoka wapi Jaji alisema
alihesabu kura hizo walizopata wagombea wa vyama 16 na kubaini ni kosa tu la
kibinadamu na halina uhusiano wowote na Mnyika.
Akizungumza nje ya Mahakama baada
ya uamuzi huo wa Mahakama, Mnyika alisema kwasababu mahakama hiyo ndiyo ya
mwisho kuondolewa kwa rufaa hiyo kunathibitisha alishinda kihalali na yeye ni Mbunge
halali wa jimbo hilo kama ilivyothibitishwa katika Mahakama Kuu.
Alisema, siku chache
zilizopita wakili Maige aliwasiliana na wakili wake Edson
Mbogoro akiomba kuondoa rufaa hiyo mahakamani na kusamehewa gharama za uendeshaji
wa rufaa hiyo.
Mnyika alisema amemsamehe
Ngh’umbi kulipa gharama za uendeshaji wa rufaa hiyo lakini gharama za kuendesha
kesi ya msingi ambayo hukumu yake ilitolewa Mahakama Kuu bado iko pale pale.
Aliongeza kuwa licha ya kuwa kesi
hiyo ilichukua miaka miwili tangu ilivyofunguliwa
mwaka juzi aliendelea kuwatumikia wananchi bila kujali kama kuna kesi
mahakamani.
Wafuasi wa Chadema walikuwa
wamefurika nje ya mahakama hiyo wakionesha ishara yao ya kunyoosha vidole
viwili hewani huku wengi wao wakisema wamefurahishwa sana na uamuzi wa Ngh’umbi
kwa kuwa walimchagua mbunge huyo kihalali.
Walitoka katika eneo hilo
wakiandamana, hata hivyo walipofika
katika maeo ya Posta mpya Mkuu wa Kituo cha Kati cha Polisi , Suzana
Kaganda aliwataka kutawanyika katika eneo hilo kwa kuwa hawakuruhusiwa kufanya
maandano kutokana na ugeni uliopo nchini kwa sherehe za Uhuru.
Mnyika aliwataka wafuasi hao
kutii amri hiyo na hivyo walitawanyika na wengine walipanda daladala.
Katika hatua nyingine, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (CHADEMA), Eddo Mwamalala, amedai kitendo cha Katibu Mkuu wa Chama
hicho Taifa Dk Wilbroad Slaa kukiri kuwa anamiliki kadi ya CCM kimewadhalilisha
huku akimtaka ajiuzuru wadhifa alionao kwa ajili ya kulinda maslahi ya chama
hicho.
Mwamalala ambaye amewahi kuwa
Katibu wa Chama hicho katika Mkoa wa Mbeya kabla ya kusimamishwa nafasi hiyo na
Dk. Slaa alisema kitendo hicho kinaonesha wazi namna kiongozi huyo alivyokosa
uadilifu na huruma kwa Watanzania walioweka rehani maisha yao ili kuliletea
Taifa maendeleo.
Akizungumza na vyombo mbalimbali
vya habari Jijini Dar es salaam jana, Mwamalala alisema kwa kufanya hivyo, Dk
Slaa pia anakuwa amekiuka sura ya tano ibara ya kwanza ya Katiba ya Chama hicho
inayomtaka mwanachama yeyote wa chama hicho kutokuwa mwanachama wa chama
kingine baada ya kujiunga na Chadema.
“Dk Slaa ni kiongozi na jicho la
Chadema, kitendo cha yeye kukiri hadharani kuwa anamiliki kadi ya CCM,
kimekitia doa chama chetu na kinaonesha udhaifu tulionao hivyo kwa maslahi ya chama
hiki ni vizuri akajiuzuru na kuwapisha watu wenye sifa ya kuwa viongozi wa
kweli katika chama,” alisema Mwamalala.
Hivi karibuni, Slaa kupitia
mkutano wake na waandishi wa habari, alikiri kumiliki kadi ya CCM baada ya Katibu
wa Itikadi na Uenezi wa CCM Nape Nnauye kutamka hadharani kuwa Katibu huyo wa
Chadema anamiliki kadi ya CCM.
Kutokana na kitendo hicho cha Dk
Slaa, Mwamalala alisema ni ni vyema Katibu huyo akajitathimini mwenyewe kama
anatosha kuendelea kuongoza chama na wanachama wakati anavunja na kudharau Katiba
yake.
“Nawaomba Watanzania wote
wanaoiunga mkono Chadema, tuungane kwa pamoja kama kweli tumedhamiria kushika
dola Mwaka 2015, watu kama Dk Slaa ni ndumilakuwili hawatufai tena bali wapo
wakitumia shida za wananchi kujipatia umaarufu wa kuendesha maisha yao huku
wakiacha wananchi wakiteseka,” alisema Mwamalala.







0 comments:
Post a Comment