Thursday, December 6, 2012

Maonyesho ya Jua kali Yafunguliwa Rasmi

MAONESHO ya 13 ya Nguvu Kazi/Jua Kali kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), yamefunguliwa juzi mjini hapa huku Makamu Spika wa Bunge la Burundi, Jean Kabura akisema maonesho hayo yana nia ya kuendeleza shughuli za sekta binafsi na kuongeza ajira kwa wajasiriamali.


Kabura alisema maonesho haya yanaendana na sera ya Afrika Mashariki ya kuendeleza viwanda ambayo ilipitishwa na Wakuu wa Nchi Wanachama katika mkutano wao wa kilele mwaka 2011 mjini hapa.


Aidha, ameongeza kuwa maonesho haya yatawasaidia vijana kujikita katika sekta isiyo rasmi ili kuongeza ajira kwa vijana  na hatimaye kuondoa kabisa umasikini wa kipato.


Makamu Spika aliwaomba wafadhili kuangalia bidhaa za wajasiriamali ili kutafuta njia za kuwasaidia kuongeza ubora wa bidhaa hizo na kuwatafutia masoko. Aliwashukuru waandaji wa maonesho kwa maandalizi mazuri na kufanikisha shughuli nzima ya uzinduzi.


Akitoa salamu kwa niaba ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Dk James Nzagi ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Burundi kwa maandalizi mazuri ya maonesho na kwa mapokezi mazuri kwa washiriki wote waliofika Bujumbura.


Aidha, aliwashukuru watumishi wa mipakani kwa ushirikiano waliouonesha kwa wajasiriamali wa Tanzania kupita kwa usalama na mali zao bila kusumbuliwa na kusema kuwa hii ni ishara ya kuonesha ushirikiano ulio imara katika nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.


Dk Nzagi alisema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayachukulia maonesho haya kama njia ya kubadilisha Tanzania kuwa taifa la uchumi wa kati na unaoendeshwa na viwanda.


Alisema kwa kuzingatia umuhimu wake kwa Watanzania, Serikali imeendelea kuwasaidia wajasiriamali wa sekta isiyo rasmi kushiriki maonesho haya ili kukuza shughuli zao na kuimarisha ajira zao.


Katika maonesho haya, Tanzania ilipewa nafasi 185 za wajasiriamali kushiriki. Wajasiriamali 87 ndio walioshiriki wakiwa na bidhaa mbalimbali ambazo ni pamoja na nguo za batiki, vyakula vya kusindika, bidhaa za ngozi, dawa za asili, dagaa wa kukaushwa, mafuta ya ubuyu na vikapu vya kushona.


Maonesho ya 13 ya Nguvu Kazi/Jua Kali ya Afrika Mashariki hufanyika kila mwaka kwa mzunguko katika kila nchi wanachama wa EAC baada ya kufunguliwa rasmi Novemba, 1999 mjini Arusha. Maonesho hayo kwa mwaka huu yanafanyika Burundi ikiwa ni mara ya kwanza kufanyika nchini humo.


Maonesho hayo yana lengo la kukutanisha wajasiriamali wadogo kwa ajili ya kubadilishana uzoefu, kuwajengea mtandao wa kibiashara, kukuza vipaji vyao pamoja na teknolojia.


0 comments:

Post a Comment